Achilia Na Songa Mbele

Mambo ya nyuma yasikufanye ushindwe kuifurahia leo yako au kupanga mipango kwa ajili ya kesho yako. Hakuna ambaye hajawahi kuumizwa iwe ni maisha/ mtu / watu au hali. Kinachotofautisha ni uamuzi wa kuachilia maumivu na machungu ya nyuma na kusonga mbele. Kuendelea kuyashikilia na kuyabeba kama bango haiondoi uhalisia kuwa yametokea wala hakufanyi leo yako kuwa nzuri.

Tambua kuwa maisha yako ni jukumu lako na si mwingine yeyote. Haijalishi umeumizwa vipi, unawajibika kuishi maisha yako kwa furaha na kufanya bidii ili kesho iwe bora zaidi. Aliyekukosea au kukusababishia maumivu hawajibiki kukupa furaha wala kukuondolea maumivu, ni jukumu lako asilimia mia. Amka sasa, jikung’ute maumivu yote na uchungu wa yaliyopita na usonge mbele.

Si kwa uweza wala nguvu zetu bali kwa msaada wa Mungu.

Malengo Ya Mwaka

Unapoanza Mwaka ni wakati muafaka wa kuweka malengo unayotaka kufanikisha katika Mwaka husika na mikakati ya utekelezaji. Bila kuweka malengo unawezakuta mwaka unaisha na hakuna kitu umekamilisha.

Nimeweka mtiririko wa maswali yatakayokusaidia kukuongoza jinsi ya kuweka malengo katika maeneo mbalimbali ya maisha kama kiroho, kiuchumi, afya, familia n.k

Download Malengo Ya Mwaka

Jinsi Ya Kufanya Maono Yako Yawe Hai

cropped-wpid-gardenofgrace.jpg

Bila ya kuwa na maono ya wapi unaelekea ni rahisi kuchukuliwa na upepo na kupelekwa usikokutazamia. Maono yatakufanya ujue ni nini ufanye kwa ajili ya Mungu na maisha yako kwa ujumla.

Mithali 29: 18 

Maono yako kwa ajili ya kazi ya Mungu ni lazima yaendane na agizo kuu alilolitoa Bwana Yesu kwa wote wanaomwamini.

Marko 16:15
 Akawaambia, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri injili kwa kila kiumbe.

Ni lazima mara zote agizo hili liwe ndani yako ili unapoendelea na maono yako usijeenda mbali na agizo hili.

Shetani hujaribu kuyafisha maono yako na usipokuwa mwangalifu atayapoteza kabisa. Yeye mara zote hutaka kituzuia kuyafanya mapenzi ya Mungu, anajua akiyaua maono yetu hatutaweza kuifanya kazi ya Mungu kwa ukamilifu.

2Korintho 2:11 Shetani asije akapata kutushinda; kwa maana hatukosi kuzijua fikira zake.

Mambo yafuatayo shetani huyatumia kuua maono yetu:

1. Dhambi ambazo hazijatubiwa
Isaya 59:9-12 Mistari hii inaonyesha kuwa dhambi isipotubiwa hupofusha macho ya rohoni hivyo hutaweza kuyaona maono yako. Dhambi inakuweka mbali na utukufu wa Mungu.

2. Uhusiano uliovinjika katika mwili wa Kristo 
Tunaporuhusu makosa ya ndugu zetu katika Kristo kuzaa uchungu badala ya kusamehe, tunaruhusu shetani kuyafunga macho yetu ya kiroho na hivyo kushindwa kuiona njia ya kuelekea kwenye maono yetu.

3. Tamaa ya mambo yanayoonekana

Zaburi 119:37 Unigeuze macho yangu nisitazame yasiyofaa, unihuishe katika njia yako.

Ukiangalia sana mambo ya dunia na tamaa zake utajikuta unayasahau maono yako na kubaki umefungwa na mambo hayo.

4. Kuangalia sana mambo ya nyuma.
Unapoacha kutazama mbele unapoelekea na kuweka nguvu na akili yako yote katika mambo ya nyuma yaliyopita, utapoteza kusudi lako na maono yako.

Mwanzo 19:26 Lakini mkewe Lutu akatazama nyuma yake, akawa nguzo ya chumvi.

Wafilipi 3:13 Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele.

5. Kutumia muda mwingi kuangalia matatizo 
Shetani hujaribu kutufanya tuangalie tu matatizo tuliyonayo na yale yanayoweza kutokea tunapoyafanyia kazi maono yetu hivyo kutuondolea imani ya kuyakamilisha. Biblia katika kitabu cha hesabu inaelezea habari za wapelelezi kumi waliorudi na habari za kukatisha tamaa katika kuiendea nchi ya ahadi maana waliangalia zaidi matatizo na kupoteza maono yao ya kuingia nchi ya ahadi.

Joshua na Kaleb waliona zaidi ya matatizo, waliuona ukuu na uaminifu wa Mungu. Hawakuwa na hofu yoyote hivyo waliweza kuingia nchi ya ahadi (kukamilisha maono yao) maana walimwamini Mungu. Petro alijaribu kutembea juu ya maji lakini alipoona mawimbi akasahau Yesu aliyekuwa mbele yake akimwambia njoo, akaweka akili kwenye mawimbi akaanza kuzama.

Ili tuweze kuyafanikisha maono yetu ni lazima tuwe na uhusiano na ushirika wa karibu na Roho Mtakatifu.

Ubarikiwe na BWANA Yesu.

Usikubali Kufungwa na Yaliyopita

2911121736_15728ac5f0

Unapoamua kumfuata na kumuishia Mungu, maisha yako ya zamani hayawezi kukuharibia wala kuwa ndio dira ya maisha yako ya sasa na baadaye. Usikate tamaa kuwa hutaweza kufanikiwa maana wewe umezaliwa katika shida, umetenda maovu sana au ukadhani umekuja duniani kwa bahati mbaya. Kila mmoja amezaliwa kwa kusudi la Mungu. Mungu anampango kamili wa maisha yako iwe umezaliwa mtoto wa nje, umezaliwa mimba ya utotoni, umezaliwa baada ya mzazi wako kubakwa, n.k. upo kwa kusudi la Mungu.

Sulemani alizaliwa baada ya Daudi kumchukua mke wa uria na kumuua uria hakini hiyo haikuondoa mpango wa Mungu juu ya sulemani. Peres alizaliwa baada ya tamari kujifanya kahaba na kulala na mkwe wake, lakini haikuzuia uzao wa Peres kuja kuwa uzao wa Bwana Yesu. Rahabu alikuwa kahaba, pale alipoamua kuungana na watu wa Mungu, kizazi cha Yesu kilipitia na kwake pia.

Usiangalie past yako, mwangalie Mungu na neno lake na uaminifu wake. Tafuta kulijua kusudi la Mungu katika maisha yako na uliishi. Yesu atabadili past yako ngumu kuwa kesho yenye ushindi na furaha.

Acha Kujihurumia Na Kulalamika

Kuna mtu aliniandikia message analalamika kuwa maisha yake yamekuwa ni ya mateso matupu, amekuwa mtu wa kuhangaika kwenye nyumba za watu mara leo anaishi na huyu mara na yule na anaona kuwa amezaliwa ili apate shida. Nilimtia moyo na kumpa maneno ya kumsaidia. Ila nimeona leo niliongelee jambo hili hapa.

Watu wengi sana wanasumbuliwa na hali ya kukosa shukurani. Ukimwambia mtu hivyo anaruka hapana mimi nashukuru kwa kila ninalopewa, ila ukweli unabaki kuwa tatizo hili linasumbua wengi. Na linaongezewa na hali ya kuona kuwa mtu mwingine ndiye anajukumu la kukupa furaha na kufanikisha maisha yako mfano mzazi, ndugu, rafiki, mume, mke n.n.

Nilikutana na mtu aliyenifundisha jambo kubwa sana kutokana na maisha yake,. Niliposikia habari za maisha yake nilijua nikikutana naye atakuwa mtu mwenye kusononeka, huzuni, anayejiurumia na kulaumu wengine lakini haikuwa hivyo. Alikuwa mtu aliyejaa furaha, mkarimu, anayepambana kuyakomboa maisha yake bila kuangalia changamoto lukuki zilizomzunguka na anayewajali na kuwasema vizuri wale ambao kwa uhakika walistahili kumsaidia lakini walimtenga.

Nikajifunza kuwa hata ukijihurumia na kulaumu mazingira yaliyopelekea hali yako kuwa hivyo kamwe huwezi kuibadili, unapaswa kumshukuru Mungu kwa vile ulivyonavyo na kuweka bidii, narudia bidii ili kuyakomboa maisha yako. Usiishie kuota, bali fanya kazi kwa uwezo wako wote. Mshukuru Mungu una watu wanaoweza kukupa mahali pa kulala hata kama ni wiki moja, mshukuru Mungu unapata chakula kuna ambao hata hizo nyumba za kuzunguka leo kwa huyu kesho kwa huyu hawana. Changamoto zako ziwe daraja la kukuvusha kuelekea mafanikio na sio utelezi kukupeleka shimoni.

Wewe Ni Wa Thamani

932402163-mother-holding-a-baby-with-head-on-shoulder
Pongezi nyingi kwako msichana uliyepewa mimba na kutelekezwa lakini hukuitoa bali uliamua kuilea na kuendelea kumlea mtoto wako peke yako bila hata ya msaada wa baba wa mtoto. Wamama wengi ambao hulea mtoto au watoto bila kuolewa maranyingi huonekana kama hawapo sawa kulingana na mfumo wa jamii. Jamii imekuwa ikiwa judge bila kujua nini wamepitia na wanapitia. Ni ukweli usiopingika kuwa watoto wanapaswa kulelewa na wazazi wawili lakini hii siyo sababu ya kumdharau msichana anayalea mtoto mwenyewe maana hujui nini kimepelekea hali hiyo.

Mungu awabariki sana na awakumbuke pamoja na watoto wenu. Usikate tamaa wala kujenga chuki na kisasi na baba wa mtoto, wewe endelea kuangalia maisha ya mtoto wako na kuboresha maisha yako na hakika Mungu hatakuacha na atakupa haja za moyo wako. Sisi wenye ndugu na marafiki ambao ni single mothers tujue wanatuhitaji kuwakubali, kuwatia moyo na kutowajudge.  Kama hajaamua kukuambia baba wa mtoto heshimu maamuzi yake na sio kila saa kumsumbua kwa maswali.

Thamani Ya Mwanamke

Mungu aliona si vyema adamu aishi peke yake akaamua kumtafutia msaidizi wa kufanana naye. Wanawake tumeumbwa kwa kusudi kamili la Mungu na tunajukumu la kuwa wasaidizi. Nafasi ya mwanamke katika jamii, familia, ndoa, kanisa na taifa ni kubwa sana. Angalia jinsi wanawake wanavyohangaika na watoto, kuanzia wakiwa tumboni hadi wakiwa watu wazima. Mwanamke ni mjenzi wa familia, mwanamke ni muunganishi wa familia na mwanamke ni mrutubishaji wa familia.

Moyo wa mwanamke unauwezo mkubwa sana, yani hawa nakaa nafikiria moyo wa mwanamke nashindwa kuuelewa kabisa, wanawake wanatendwa kila siku lakini wanasamehe, wanajitahidi kuachilia japo ni ngumu na wanaamua kuendelea kutenda mema. Unakuta mama anagundua mumewe anatembea nje, na hata anafikia kulala nje, mama huyu atalia, ataumia lakini atampikia chakula, atamfulia, atamuombea ataamua kumsamehe na hata akiletewa mtoto wa nje anamtunza. Hivi ni wanaume wangapi wanaoweza kuwasamehe wake zao wanaotembea nje? Na pale anaporudia na kurudia na wakati mwingine kulala nje???

Mungu awakumbuke wanawake wote.
Mungu asikie kilio chako unacholia ndani ya shuka na bafuni.
Mungu akuonekanie na kukurejeshea furaha ya maisha.
Mungu akutetee wewe ukiyepewa mimba na kuachwa.
Mungu akutunze wewe uliyetelekezwa na mume na ukaachiwa watoto.
Mungu awe mume wa wajane wote.
Mungu ailainishe mioyo ya waume wote, waitambue thamani ya wake walionao, Mungu awafunike macho yao wasione wengine zaidi ya wake zao.

Mungu alituumba kwa kusudi, tufurahie uanamke wetu na kamwe tusikubali changamoto za maisha zituondolee furaha. Mungu aliona dunia haitakuwa njema bila sisi ndio maana akaamua kutuumba, sisi ni wa thamani saanaaa….

Ongea Habari Za Mungu Na Watoto Wako

children_field

Shalom

Je Mungu ni sehemu ya mazungumzo yako ya kila siku na watoto wako? Au unakwepa kuongea nao habari za Mungu? Watoto wako wanamuona Mungu katika maneno yako ya kila siku? Kitu unachokithanimi utawekeza muda wako, mali na hata nguvu zako. Watoto wako waone jinsi unavyowekeza kwa Mungu katika kulisoma neno lake, kuomba, kuhudhuria kanisani na kutumika katika kazi ya Mungu.

Tunapozungumza ukuu wa Mungu na watoto wetu katika maisha ya kila siku tunawajengea hazina kubwa ya imani kwa Mungu wao ambayo watakuwa nayo siku zote. Pamoja na kuwahamasisha kupata maksi nzuri darasani, kujihusisha na michezo na kufanya kazi za nyumbani hakikisha unawafundisha kumtumikia Mungu katika umri wowote walionao. Neno la Mungu liwe sehemu ya maisha yako na watoto wako siku zote.

KumbuKumbu 11:18-19 “Kwa hiyo yawekeni maneno yangu mioyoni mwenu na rohonu mwenu; yafungeni yawe dalili juu ya mikono yenu, nayo yatakuwa kama utepe katikati ya macho yenu. Nayo yafunzeni Vijana vyenu kwa kuyazungumza uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo

Kusamehewa Sio Kibali Cha Kuendelea Na Makosa

lady_sea

Kusamehewa hakukufanyi wewe uendelee na makosa eti sababu unajua kuwa utasamehewa. Unapoomba msamaha maanisha unachokisema na dhamiria kutoka moyoni kutokurudia tena kosa na epukana na mazingira yaliyokufanya ukatenda kosa hilo. Kuna watu kwa makusudi wanafanya makosa na kuyarudia wakijua kuwa wenzi wao watawasamehe sababu ni wepesi kusamehe. Unakuta mtu anafanya uzinzi, anasamehewa, anaendelea na wala hajali, au mtu anampiga mke wake, anasamehewa na anaendelea tena na tena.

Kusamehe hakumaanishi kuwa mtu upo tayari kuhatarisha maisha yako. Unaweza kumsamehe mtu anayekupiga lakini ukajitenga mbali naye sio sababu hujamsamehe bali kwa usalama wako watoto kama wapo na yeye pia maana anaweza kukudhuru akaishia gerezani, mpaka pale atakapoamua kweli kubadilika. Kusamehe hakumaanishi kuishi katika mateso.

Nawewe uliyesamehewa na kisha ukaendelea na makosa ukijua utasamehewa kumbuka ghadhabu wa Mungu ipo na hakika usipogeuka na kuiacha njia yako mbaya hauwezi kuiepuka!

Bible Study

loving_arms2

SOMO: HANA – UTHABITI KATIKA MAJARIBU

MAANDIKO: 1 SAMWELI 1:1-28; 2:1-10

Hana alikuwa ameolewa na mtu aitwaye Elikana. Elikana alikuwa na wake wawili wa kwanza akiitwa Penina na wa pili Hana. Penina alikuwa amejaliwa watoto wa kike kwa wa kiume lakini Hana yeye hakuwa na mtoto. Hali hiyo ilikuwa inamuumiza sana, mumewe alijitahidi kumuonyesha upendo na kujali ila bado moyo wake ulikuwa na mzigo mkubwa. Penina hakuwa msaada bali alizidisha maumivu ya Hana kwa kumchokoza kwa sababu ya kukosa mtoto.

Hali hiyo ya maumivu ya kukosa mtoto na kuchokozwa ilimpelekea Hana kuwa na maombi mazito mbele za Mungu. Hapa tunaona jinsi Hana alivyokuwa mwanamke thabiti wa imani, alikuwa na kila sababu ya kulalamika na kuona kama Mungu amemsahau au kuingia kwenye malumbano na Penina. Yeye alitambua kuwa mwenye uwezo wa kumpa mtoto ni Mungu na kamwe hawezi kushindwa, aliingia kwenye maombi na kukazana na maombi akiamini Mungu atafanya. Alimwekea Mungu nadhiri kuonyesha ni jinsi gani anahitaji mtoto.

Tunaona pia akiwa kwenye maombi mazito hadi sauti ikawa haitoki, kuhani Eli alidhania amelewa. Unaweza ukaona ni jinsi gani Hana alikuwa anaomba kwa uchungu, na alijisikiaje vibaya baada ya kuhani kuanza kumgombeza kuwa atalewa hadi lini wakati yupo kwenye majonzi mazito. Lakini majibu yake yanaonyesha kuwa Hana hakuruhusu maneno yale yamuondoe kwenye kusudi la maombi yale, hakuruhusu maneno yale ya kukatisha tamaa yaweke uchungu ndani yake bali aliendelea kuwa mnyenyekevu akimwamini Mungu. Unaweza kuwa unapitia magumu sana katika maisha halafu wale unaowategemea wakutie moyo na kukufariji ndio wakawa wa kwanza kukutuhumu na kukulaumu.

Tujifunze kwa Hana, usiyaweke moyoni maneno hayo wala usikubali yakutoe kwenye maombi yako kwa Mungu. Vile vile hapa tunaona shutuma za Eli hazikumfanya Hana amuone hafai na kutokumsikiliza. Aliendelea kumheshimu kama kuhani na alisikiliza neno lake na kulifanyia kazi. Wengi wetu hapa tungeshindwa. Tujifunze kwa mwanamke huyu mwenye imani thabiti. Endelea kumwamini Mungu, endelea kumimina moyo wako mbele za Mungu na hakika wakati utawadia na Bwana atatenda kwa utukufu wake. Wakati wa Bwana utawadia tu, Bwana mwenyewe atawanyamazisha wanaokushutumu na kukuchokoza kwa sababu ya hali uliyonayo. Usitafute wewe kuwanyamazisha, tujifunze kwa Hana alivyokabiliana na Penina bila kujibizana naye.

1 Samweli 1 : 20 – Ikawa, wakati ulipowadia, Hana akachukua mimba na kuzaa mtoto mwanamume; akamwita jina lake Samweli, akisema, Kwa kuwa nimemwomba kwa Bwana.

Pia tunaona kuwa Hana alikuwa mwaminifu kumtolea Mungu nadhiri aliyoiweka. Pamoja na kuwa alihitaji mtoto sana lakini hakuacha kumpeleka hekaluni kama alivyoahidi kwenye maombi. Unapokuwa katika maombi kama huna uhakika na uwezo wa kuitumiliza nadhiri ni vena usiiweke. Uwekapo nadhiri yako kwa Mungu hakikisha umeiondoa pale Mungu anapo kutendea.

Kumbukumbu la Torati 23 : 21 – Utakapoweka nadhiri kwa Bwana, Mungu wako, usiwe mlegevu katika kuiondoa; kwa kuwa Bwana, Mungu wako, hataacha kuitaka kwako; nayo hivi itakuwa dhambi kwako.

Mhubiri 5 : 4 – 5 Wewe ukimwekea Mungu nadhiri, usikawie kuiondoa; kwa kuwa yeye hawi radhi na wapumbavu; basi, uiondoe hiyo uliyoiweka nadhiri. Ni afadhali usiweke nadhiri, Kuliko kuiweka usiiondoe.

Tunamaliza somo letu kwa wimbo wa sifa kutoka kwa Hana. Hana alimwomba Mungu kwa machozi na alipotendewa alirudi na wimbo wa shukrani. Je umemshukuru Mungu kwa yale amekutendea au unaona ni sababu ya maombi yako mengi na mazito ndio maana umepata? Ukisoma sura ya pili hapo utaona shukrani zake kwa Mungu. Ameonyesha kabisa kuwa ni Mungu tu aliyetenda na mwenye nguvu, yeye hana la kujisifia. Tujifunze katika hili.

Maswali

1. Nini kilimpa Hana uchungu mwingi? Je ni maneno ya Penina.? Shutuma za Kuhani? Kutokuwa na mtoto?

2. Alikabiliana vipi na maumivu na uchungu ndani yake?

3. Unadhani ilikuwa rahisi kukabidhi mtoto kwa kuhani baada ya kumsubiri kiasi hicho?

4. Ni kiasi gani maneno ya watu ya kukatisha tamaa na kuvunja moyo yamekuathiri na kukuzuia kufikia ndoto zako?

5. Pale Unapokuwa na hitaji kubwa ila hauoni kama linapatikana huwa unakabiliana vipi na hali hiyo?

6. Je pale kiongozi wako wa imani anapokuonyesha kutokuamini unayoyafanya na kukushutumu huwa unakabiliana vipi? Je huwa unaendelea kumsikiliza akisema maneno ya Mungu?

7. Umejifunza nini kupitia maombi ya shukrani ya Hana?

Limeandaliwa na womenofchrist.wordpress.com