Baada ya kutoa orodha ya vitu vya kuhakikisha unakuwanavyo unavyoenda kwenye fungate (honeymoon), nimegundua kuwa maharusi wengi hawaelewi ni muda gani wa kujiandaa na kuandaa mahali pa kwenda kwa ajili ya fungate. Fungate ni kitu muhimu sana kwa ajili ya watu wanaooana hivyo ni lazima jambo hili lipewe kipaumbele linachostahili.
Pale mnapoanza mipango ya harusi ndio wakati muafaka wa kuanza kupanga kuhusu jambo hili. Ni muhimu kila mmoja wenu akawa huru kusema anataka mahali pa aina gani na mkubaliane kwa pamoja kwa kuzingatia vigezo mbalimbali. Kuna wakaka wengine wanapenda kuwafanyia wenzi wao surprise, hata kama ni surprise ni vizuri ukajua anapendelea nini usije ukamvunja moyo siku us kwanza ya ndoa yenu.
Mambo muhimu ya kuzingatia ni pamoja na:
1. Gharama ziwe zinalingana na uwezo wenu.
Hapa ni lazima utambue kuwa jambo hili ni la mara moja hivyo ni bora uwe na harusi ya kawaida ili muweze kupata hela nzuri ya kwenda mahali pazuri kwa ajili ya fungate.
2. Eneo lililotulia mbali na maeneo mnayoishi
Haitakuwa vyema kuamka asubuhi kwenda kupata kifungua kinywa siku ya kwanza ya ndoa yenu na kukutana na mama mkwe. Tafuta mahali patulivu, pembezoni mwa mji mbali na mahali mnapoishi. Kama mnampango wa kwenda mji mwingine msisafiri mara baada ya harusi, mpunzike kwanza angalau siku mbili ndipo msafiri.
3. Msitumie simu zenu angalau kwa wiki ya kwanza ili mpate muda wa kuwa na faragha ya kutosha. Unaweza kuwasha simu ukakutana na mambo ya kikazi au kijamii yakakuondolea furaha au concentration. Fungate no kwa ajili yenu kuwa wawili pamoja na kufahamiana kwa undani. Inashangaza sana kuona mtu anafunga ndoa jumapili halafu jumatatu unamkuta online facebook. Unapata wapi huo muda? Na kwanini? Fungate ni jambo la kulidhamini sana, ni muda wa kumpa mwenzi wako muda wako wote na usikivu wako wote na ukaribu wote. Ukiwa honeymoon inakubidi akili yako yote ijae mwenzi wako na maisha mnayoyaendea, achana na simu utaikuta tu baada ya kuweka msingi imara wa ndoa yako.
Kuna watu wanahoji umuhimu wa kwenda hotelini kwa ajili ya fungate. Mwili wa binadamu unahitaji kula, kukaa mahali safi na kuvaa nguo safi. Sasa mkienda nyumbani itabidi muwe na muda wa kupika, kufua na kufanya usafi, mambo haya yanawapunguzia muda wa kuwa intimate pamoja ukizingatia ndio mara ya kwanza. Hivyo ni vyema mkawa hotelini ili mpate muda mzuri wa kuwa pamoja.