Panda kwa Machozi Utavuna Kwa Furaha

ZAB. 126:5-6
“Wapandao kwa machozi Watavuna kwa kelele za furaha.  Ingawa mtu anakwenda zake akilia, Azichukuapo mbegu za kupanda. Hakika atarudi kwa kelele za furaha, Aichukuapo miganda yake.”

Kupanda siku zote ni kazi ngumu. Kwanza ni lazima uamke asubuhi na mapema, ubebe mbegu na jembe, utembee kwenye baridi kuelekea shamba ambalo limejaa matope maana watu hawapandi wakati wa kiangazi, uiname shambani siku nzima au siku kadhaa ukipanda mbegu zako. Sio zoezi la kufurahia au kuchekelea lakini ni la muhimu sana kama unataka kuvuna.

Siku ya kuvuna ni siku ya furaha, siku ya kuhesabu utajiri, siku ya kuhesabu matunda ya jasho, siku ambayo taabu ya kupanda inazaa matunda, pamoja na kwamba utachoka lakini unakuwa umejaa furaha maana sasa mavuno umeyapata. Lakini huwezi kuvuna bila kupanda, lazima upande ili utazamie kuvuna. Usione wengine wanapanda ukavuta shuka halafu ukasubiri nawe ukavune.

Leo nakutia moyo wewe uliye kwenye hatua ya kupanda, Usikate tamaa jua ipo siku utavuna kwa kelele za furaha. Unaweza kuwa unapanda kwenye elimu, biashara, ujasiriamali, ufugaji kazini kwako, uwekezaji, ujenzi, huduma n.k. wewe endelea kupanda kwa bidii, panda mbegu nyingi kadiri uwezavyo wala usiwe mvivu. Mbegu siku zote ni chache na mavuno ni mara 100, hivyo panda, panda, panda. Na wewe unayesubiri kuvuna wakati hutaki kupanda kwa machozi tambua kuwa hakuna kuvuna bila kupanda. Ukitaka siku ya mavuno nawe ushangilie chukua mbegu shika njia nenda shambani ukapande.
Mbarikiwe.

3 thoughts on “Panda kwa Machozi Utavuna Kwa Furaha

  1. Asante Mtumishi kwa neno hili litakaloponya wengi. Ubarikiwe.
    Pia nawakumbusha watu wa Mungu, bunge la kamati ya katiba ndiyo limeanza leo, hebu tujumuike pamoja kuomba kwa ajili ya maamuzi yatakayopitishwa, mwovu asijepanda vitu vyake katika sheria za nchi yetu.
    Tushiriki kwa maombi kila siku ya kikao mpaka maamuzi ya mwisho yatakapopitishwa, tukiwa na imani kwamba Mungu tunayemuamini hana mipaka hata tusipokuwepo mle bungeni tunaye Roho wa Bwana ambaye yupo atatuwakilisha kusimamia maamuzi yenye manufaa kwa nchi yetu.

  2. Amen,
    nimetiwa nguvu na ujumbe wako kwa vile nina sehemu nyingi za kupanda mbegu na ninaona kwa akili na nguvu zangu siwezi ila kwa Bwana Yes yeye anitiae nguvu nitashinda na siku moja nitavuna.

  3. Shalom, naitwa Kaiza Kilango nakiri kubarikiwa na ujumbe wa kupanda ni neno linaloishi na kutumiza wapendwa kupenda kufanya kazi. Mungu akubariki mpendwa

Leave a comment